LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Aug 22, 2017

RIDHIWANI-AKEMEA UFUGAJI HOLELA AMBAO UHARIBU RUTUBA





Picha mbalimbali zikimuonyesha mbunge wa jimbo la Chalinze ,Ridhiwani Kikwete ,wakati wa makabidhiano ya pikipiki kumi kwa maafisa mifugo katika halmashauri ya Chalinze kwa lengo la kufikia wafugaji kuwapa elimu za kufuga kisasa na kuondokana na migogoro na wakulima,makabidhiano yaliyofanyika huko Lugoba.(picha zote na Mwamvua Mwinyi )
Na Mwamvua Mwinyi,Chalinze
MBUNGE wa jimbo la Chalinze ,Ridhiwani Kikwete,amekabidhi pikipiki kumi ,zilizogharimu sh.Mil.22.5 kwa maafisa mifugo wa kata ,ili waweze kuwafikia wafugaji wote,kupeleka sera ya kufuga kisasa na kuondoa migogoro na wakulima.
Aidha amekemea tabia inayofanywa na baadhi ya wafugaji ya kufuga kizamani kwa kuswaga makundi ya ng’ombe kwenye eneo moja hali inayosababisha kuharibu rutuba.
Akikabidhi pikipiki hizo,huko Lugoba Ridhiwani alieleza , vyombo hivyo vya usafiri vikatumike kusimamia majukumu waliyonayo badala ya kuvitumia kwa matumizi yao binafsi.
Aliwataka jamii ya wafugaji kuachana na mtazamo hasi wa kufuga kizamani mifugo lundo isiyo na tija pamoja na kuingia katika maeneo ambayo hayajatengwa kwa ajili yao.
“Sisi hapa ni kazi tuu mkasimamie majukumu yenu ipasavyo ili kuondokana na changamoto zinazowakabili wafugaji na muwafikie wanannchi muwaeleze juu ya ufugaji bora “
“Eneo zima linageuzwa machungio,wafugaji wafuge kwa kuheshimiana hivyo muwafikie walio mbali muwape elimu hasa ya ufugaji bora.visingizio vimekwisha kuwa hamna usafiri, matarajio yangu ni mtaenda kutekeleza ilani  ya CCM”alisema Ridhiwani.
Ridhiwani ,alieleza wafugaji hasa wa kimasai wanaamini kuwa na ng’ombe wengi ndio utajiri ,waondoe dhana hiyo kwani sio sifa,wajaribu kufuga mifugo michache na kujiwekea kasumba ya kufuga kwenye mazizi.
Hata hivyo ,alimpongeza mkurugenzi wa halmashauri ya Chalinze,Edes Lukoa kwa kusimamia na kuyafanyia kazi maazimio ya madiwani ambayo huwa wakitoa .
Ridhiwani,alito mafuta  lita tano kwa kila pikipiki na kuahidi kuangalia uwezekano wa kufanya utaratibu kila mwezi kwenye posho zinazokwenda katika kata maafisa mifugo hao wataongeza japo 5,000 kwa ajili ya mafuta ya pikipiki hizo.
Kwa upande wake mkurugenzi wa halmashauri hiyo,Lukoa alisema pikipiki hizo zimenunuliwa kutokana na mapato ya ndani ya halmashauri .



Alizitaja kata zilizokabidhiwa usafiri huo kuwa ni sanjali na Vigwaza,Kibindu,Mbwewe,Talawanda,Msata,Kimange,Kiwangwa,Miono,Ubena Zomozi na Mandela.
Lukoa  alieleza kwa msimu wa bajeti 2017/2018 wanatarajia kununua pikipiki nyingine 15 kwa ajili ya watendaji na nyingine nane kwa ajili ya maafisa mifugo wa kata na vijiji .
Aliwashukuru madiwani kwa ushirikiano na CMT kwa mchango  wao mkubwa katika kutoa maazimio yaliyotakiwa yatekelezwe na halmashauri na sasa yamefanikiwa.
Lukoa alifafanua,kila afisa mifugo wa kata anayekabidhiwa pikipiki atasaini mkataba wa makubaliano na mwajiri wake na atatakiwa kuchangia asilimia 50 ambayo ni sawa na sh.bil 1.125 ya sh.bil 2.250 ambayo ni bei ya kukunuliwa atakayokabidhiwa kwa kipindi cha miaka mitano.
“Hali hiyo itasaidia kutunza pikipiki kwa kuwa itakuwa ni mali yao baada ya kumaliza kuilipia malipo wanayokatwa yatawezesha kununua pikipiki nyingine ili kuimarisha huduma za ugani’alisema Lukoa.
Nae afisa mifugo na kilimo katika halmashauri ya Chalinze ,Bagamoyo Issack Kama,alisema wapo maafisa mifugo wa kata na vijiji 26 ambao wanapaswa kutoa huduma za ushauri wa kitaalamu kwa wafugaji waliopo kwenye vijiji 68 vilivyopo humo .
Alibainisha kati ya maafisa hao wanne pekee ndiyo wana pikipiki na wengine 22 hawana  hali iliyokuwa ikisababisha kushindwa kuwafikia wafugaji na kuwapa huduma zinazostahili.
Kama alisema ili wafugaji waweze kupata mafanikio katika ufugaji wanapaswa kufuata kanuni bora za ufugaji kupitia ushauri wa maafisa mifugo wa kata na vijiji.
Katika hatua nyingine,baadhi ya maafisa mifugo waliokabidhiwa vyombo hivyo vya usafiri akiwemo afisa mifugo kata ya Talawanda Enerst Lesi,wa kata ya Mbwewe Rashid Mdemu walishukuru kupata pikipiki hizo kuwafikia wafugaji na kuboresha huduma za ugani ukizingatia wafugaji wengi wanakaa mbali.
Mdemu alielezea,kata ya Mbwewe ina vijiji sita hivyo ilikuwa ni vigumu kuvifikia vyote hasa katika kutoa elimu mbalimbali na kufanikisha zoezi la kupiga alama (chapa)mifugo ili iwe rahisi kutambulika.


Akitoa shukrani ya pamoja afisa mifugo kata ya Msata,Agripina Silau ,alisema usafiri huo wameupokea katika muda muafaka .

Alimhakikishia mbunge huyo kuwa watakwenda kuwajibika kikamilifu ili kuleta mabadiliko na kutatua changamoto ya migogoro ya wakulima na wafugaji licha ya kwasasa kuonekana kuanza kupungua.

Usajili wa mifugo na kuweka alama kwenye mifugo usafiri huu umekuja muda muafaka.

Kwa mujibu wa sense ya mifugo ya mwaka 2012,halmashauri ya Chalinze ina jumla ya ng’ombe 240,000,mbuzi 94,000,kondoo 54,000,kuku 380,000 na wanyama wengine.

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages